Na Mwandishi Wetu
Katika jitihada za kukabiliana na changamoto ya utapiamlo na lishe duni, Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, kupitia Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, imeanzisha shamba darasa la viazi lishe katika Hospitali ya Wilaya. Lengo kuu ni kuwafundisha kina mama wanaohudhuria Kliniki ya Baba, Mama na Mtoto (RCH) kuhusu umuhimu wa viazi hivyo na namna bora ya kuvilima.
Viazi lishe, ambavyo ni chanzo kizuri cha Vitamini A, husaidia watoto kuwa na afya bora, kuimarisha nguvu na kinga ya mwili, kuzuia upofu utotoni, kupunguza hatari ya vifo vya watoto wachanga, na kushusha viwango vya upungufu wa damu mwilini.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa shamba hilo hospitalini hapo, Mkuu wa Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi wa Halmashauri, Mikidadi Mbaruku, amesema kuwa iwapo wananchi watahamasika kulima zao hilo, serikali itapunguza matumizi ya fedha kununua matone ya vitamini A, fedha ambazo zinaweza kuelekezwa kwenye shughuli nyingine za maendeleo.
“Idara ya Kilimo tumeamua kuanzisha shamba hili hapa hospitalini ili kina mama mnapofika kliniki au kwa ajili ya matibabu, muweze kujifunza namna viazi hivi vinavyolimwa. Pia tunawahimiza wote wanaohitaji mbegu kuwasiliana na maafisa ugani katika vijiji vyao ili waelekezwe vizuri kuhusu upandaji na matumizi ya viazi hivi,” amesema Mbaruku.
Kwa upande wake, Afisa Lishe wa Halmashauri hiyo, Subira Swai, amesema matumizi ya viazi lishe yatapunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa vidonge vya virutubisho, na kuwataka wakina mama wanaohudhuria kliniki kutumia vyema wataalamu wa kilimo waliopo kwa ushauri.
Naye Afisa Kilimo wa Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu, Masumbuko Kwelema, amewahimiza kina mama wajawazito na wale wenye watoto wachanga kuhakikisha wanakuwa na bustani za viazi hivyo majumbani mwao kama njia mojawapo ya kuboresha lishe na afya ya familia.
HALMASHAURI YA WILAYA YA KASULU
Anuani ya Posta: S.L.P 97
Simu ya Mezani: +255-028-2810339
Simu: +255-028-2810339
Barua Pepe: ded@kasuludc.go.tz
Copyright ©2024 kasuludc . All rights reserved.