Na Mwandishi Wetu
Walimu wa Shule ya Msingi Kisuma wamewashukuru wadau mbalimbali wakiwemo wale kutoka shirika lisilo la kiserikali la Usilie Tena, kwa kuwasaidia wanafunzi wenye uhitaji kwa kuwapatia sare za shule, mikanda, na vifaa vya kujifunzia.
Akizungumza jana wakati wa tukio la ugawaji wa msaada huo shuleni hapo, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Everest Ntagaye, amesema kuwa misaada hiyo imekuwa na mchango mkubwa katika kuongeza hamasa ya wanafunzi kuhudhuria masomo, hali iliyosaidia kupunguza utoro.
“Katika siku ya leo, baadhi ya wanafunzi wamepata sare, mikanda na vifaa vya kujifunzia. Wale ambao hawajapata kwa sasa, msiwe na wasiwasi mnaweza kupata wakati mwingine Mungu akipenda. Ni muhimu tuoneshe ushirikiano kwa kutunza tunavyopata, ili kuwatia moyo wadau wetu kuendelea kusaidia zaidi,” amesema.
Kwa upande wake, Mwalimu Jackline Mringi ameeleza kuwa misaada hiyo imesaidia kuondoa hali ya kutengwa kwa baadhi ya wanafunzi, hasa wale waliokuwa wakikabiliwa na changamoto za kifamilia, jambo lililoongeza ushiriki darasani na kuboresha ufaulu.
Katika hatua nyingine, Mwalimu Yusuph Hamisi 'U Fresh' amewashukuru wadau wote wanaoendelea kuisaidia shule hiyo, akisema kuwa msaada wao umekuwa chachu ya kuongeza motisha kwa wanafunzi kupenda shule.
Akizungumza kwa niaba ya wanafunzi, Irene Jared amelishukuru shirika la Usilie Tena na wadau wengine kwa mchango wao na kuahidi kuwa atawahamasisha wenzake kusoma kwa bidii ili waweze kutimiza ndoto zao siku za usoni.
HALMASHAURI YA WILAYA YA KASULU
Anuani ya Posta: S.L.P 97
Simu ya Mezani: +255-028-2810339
Simu: +255-028-2810339
Barua Pepe: ded@kasuludc.go.tz
Copyright ©2024 kasuludc . All rights reserved.