Wakuu wa taasisi za elimu pamoja na Idara ya Afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu, mkoani Kigoma, wametakiwa kusimamia kikamilifu suala la usafi wa mazingira ili kudhibiti milipuko ya magonjwa yanayosababishwa na uchafuzi wa mazingira.
Wito huo umetolewa leo, Jumatatu Juni 2, 2025, na Afisa Mazingira wa halmashauri hiyo, Hassan Omary, wakati wa uzinduzi wa zoezi la usafi wa mazingira katika Kituo cha Afya cha Nyakitonto. Katika hafla hiyo, Omary ametoa elimu kuhusu utunzaji wa mazingira kwa taasisi na wananchi kwa ujumla, huku akisisitiza hatari ya utupaji taka ovyo.
“Usafi wa mazingira ni mojawapo ya mbinu muhimu za kuzuia kuenea kwa magonjwa, hasa kwa kudhibiti taka ambazo zinaweza kusababisha maambukizi kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine,” amesema.
Kwa upande wake, Afisa Afya wa Halmashauri hiyo, Patrick Mihayo, amesisitiza umuhimu wa usafi wa mazingira katika jamii, akieleza kuwa ukosefu wa usafi ndio chanzo kikuu cha magonjwa mengi duniani. Ameongeza kuwa kuboresha mazingira kuna faida kubwa kwa afya ya kila mtu, kuanzia ngazi ya kaya hadi jamii nzima.
Naye Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Nyakitonto, Amani Mkemwa, ameushukuru uongozi wa halmashauri na wananchi kwa kushiriki katika shughuli ya usafi, huku akibainisha kuwa kuna mikakati madhubuti ya kukabiliana na magonjwa ya mlipuko.
Miongoni mwa mikakati hiyo, amesema Mkemwa, ni pamoja na kudumisha ratiba ya usafi wa mazingira kwa njia ya huduma kama vile ukusanyaji wa taka ngumu na majitaka.
Uzinduzi huo umeenda sambamba na wiki ya mazingira duniani, ambayo mwaka huu imebeba kaulimbiu isemayo: “Mazingira Yetu, Tanzania Ijayo: Tuwajibike Sasa, Dhibiti Matumizi ya Plastiki.”
HALMASHAURI YA WILAYA YA KASULU
Anuani ya Posta: S.L.P 97
Simu ya Mezani: +255-028-2810339
Simu: +255-028-2810339
Barua Pepe: ded@kasuludc.go.tz
Copyright ©2024 kasuludc . All rights reserved.