Na Mwandishi Wetu
Matumizi ya zana za kufundishia na kujifunzia yameelezwa kuwa ni nyenzo muhimu inayomwezesha mwalimu kufundisha kwa ufanisi na kufikia malengo ya somo kwa haraka.
Zana hizo pia husaidia kubaini mahitaji ya mtoto na namna anavyojifunza, sambamba na kumpa uwezo wa kujifunza hata pasipo uwepo wa mwalimu darasani.
Hayo yameelezwa hivi karibuni wilayani Kasulu, mkoani Kigoma na Mwezeshaji wa Mafunzo ya Mradi wa Shule Bora, Sayida Mayunga, alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu.
Amefafanua kuwa matumizi ya zana yanamwezesha mwalimu kuchambua na kutumia zana kulingana na lengo mahsusi la somo husika.
“Matumizi ya zana humsaidia mwalimu kubaini mahitaji ya mtoto na kuelewa namna mtoto anavyojifunza. Mtoto anaweza kuiga au kuelewa kwa kuona vitu vilivyotengenezwa kwa kutumia zana hizo. Ikiwa aina hii ya ufundishaji itapewa kipaumbele, itakuwa mwarobaini wa changamoto ya Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) katika shule zetu.Pia itasaidia kuongeza uelewa wa wanafunzi na hatimaye kuinua kiwango cha ufaulu,” ameeleza Mayunga.
Kwa upande wake, Mwezeshaji mwingine,Halima Dalali, amesema kuwa mbinu hiyo ya ufundishaji humsaidia mtoto kuchambua vitu, kufikiri kwa kina na kuelewa jinsi kitu fulani kilivyotengenezwa na kwa kutumia vifaa gani, hivyo kumjengea fikra yakinifu.
Katika hatua nyingine, Afisa Elimu Taaluma (Msingi) wa Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu,Joseph Maiga, amewahimiza walimu kuanzisha kona au vyumba maalum vya zana vya kufundishia, iwe ndani au nje ya darasa.
“Natoa wito kwa kila mwalimu katika halmashauri kuhakikisha anaweka mazingira ya kuwa na chumba au kona ya zana. Hii itasaidia sana kuongeza ari ya kujifunza kwa wanafunzi, kupunguza utoro, na kuwajengea ubunifu kwa kuwa nao watashiriki moja kwa moja katika kutengeneza na kutumia zana hizo,” amesema Maiga.
HALMASHAURI YA WILAYA YA KASULU
Anuani ya Posta: S.L.P 97
Simu ya Mezani: +255-028-2810339
Simu: +255-028-2810339
Barua Pepe: ded@kasuludc.go.tz
Copyright ©2024 kasuludc . All rights reserved.