Na Mwandishi Wetu
Mafunzo ya siku tatu kuhusu kusoma, kuandika na kuhesabu (KKK) kwa walimu wa darasa la kwanza na la pili kutoka shule 88 zilizopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu, mkoani Kigoma, kupitia Mradi wa Shule Bora, yamehitimishwa rasmi leo.
Katika mafunzo hayo, washiriki wamehimizwa kutumia maarifa waliyojifunza kuboresha ufundishaji kwa kutumia zana mbalimbali, kwa kuwa mbinu hizo husaidia wanafunzi wa madarasa ya awali kuelewa haraka na kwa ufanisi zaidi.
Akifunga rasmi mafunzo hayo katika Chuo cha Ualimu Kabanga, Afisa Elimu Taaluma (Msingi) wa halmashauri hiyo, Joseph Maiga, amewataka walimu kuhakikisha wanayatekeleza kwa vitendo yale yote waliyojifunza, ili mabadiliko katika ufundishaji wa KKK yaonekane wazi katika vituo vyao vya kazi.
“Kutakuwa na timu ya taifa ya ufuatiliaji na tathmini kutoka kwa wawezeshaji wa mafunzo haya, itakayopitia baadhi ya shule baada ya miezi miwili ili kuona matokeo ya kile kilichofundishwa. Wanapokuja, wanataka kuona tofauti kati ya hali ya awali na baada ya mafunzo,” amesema Maiga.
Kwa upande wake, Vumilia Msukuma, ambaye alizungumza kwa niaba ya wawezeshaji wa mafunzo hayo, amewahimiza washiriki kuhakikisha wanatekeleza kwa vitendo yale waliyofundishwa kwa ajili ya manufaa ya watoto, hususan katika kupunguza changamoto za KKK na somo la Kiingereza mashuleni.
Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, Nashon Jonas, amesema mafunzo hayo yamempa mbinu mbalimbali za kukabiliana na changamoto ya KKK shuleni kwake, na ameahidi kuanzisha darasa maalum kwa ajili ya kuwashirikisha walimu wenzake maarifa aliyoyapata.
Naye Diana Nyumayo amesema kuwa mbinu zote alizojifunza katika kipindi hicho cha siku tatu atazitekeleza moja kwa moja darasani ili kuwasaidia wanafunzi kuondokana na changamoto ya KKK.
HALMASHAURI YA WILAYA YA KASULU
Anuani ya Posta: S.L.P 97
Simu ya Mezani: +255-028-2810339
Simu: +255-028-2810339
Barua Pepe: ded@kasuludc.go.tz
Copyright ©2024 kasuludc . All rights reserved.