Na Mwandishi Wetu
Katika kuhakikisha kuwa walimu wanajengewa uwezo wa kitaaluma kazini,Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma leo Jumanne Juni 3,2025 imezindua mafunzo ya siku tatu ya kusoma,kuandika na kuhesabu (KKK) kwa walimu kutoka shule 88 ndani ya wilaya hiyo.
Mafunzo hayo, yanayofadhiliwa na Mradi wa Shule Bora, yamewalenga walimu wanaofundisha darasa la kwanza na la pili,kwa lengo la kuwawezesha kukabiliana na changamoto za stadi za msingi za KKK kwa wanafunzi.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo katika Chuo cha Ualimu Kabanga,Afisa Elimu Taaluma (Msingi) wa halamashauri hiyo,Joseph Maiga amewahimiza walimu kuyatumia maarifa hayo kwa ufanisi na kuhakikisha wanayaeneza kwa wenzao ili kuongeza tija mashuleni.
“Serikali imekuwa ikifanya jitihada kwa kushirikiana na wadau ili kuondoa changamoto hii ya KKK.Mmoja wa wadau wanaotoa mchango mkubwa ni mradi wa Shule Bora,ambao umewekeza katika afua mbalimbali, ikiwemo kuwajengea uwezo walimu wa madarasa ya mwanzo," amesema.
Kwa upande wake, Afisa Elimu Vifaa na Takwimu (Msingi) wa halmshauri hiyo, Paul Joseph, amesisitiza umuhimu wa walimu kuyatekeleza kwa vitendo yale yote watakayojifunza,ili kutoa matokeo chanya oindi tathimini ya mradi itakapofanyika.
Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo,Sebastian Mkuku, amesema anatarajia mbinu mpya zitakazotolewa zitaboresha ufundishaji shuleni,hasa kupitia uzoefu kutoka shule ambazo tayari zimefanikiwa kuondoa changamoto ya KKK.
Naye Oliver Oscar amepongeza mafunzo hayo na kueleza kuwa siku tatu hizo zitakuwa na mchango mkubwa katika kutokomeza changamoto ya KKK mashuleni,kupitia mbinu bora watakazozipata kutoka kwa wawezeshaji.
HALMASHAURI YA WILAYA YA KASULU
Anuani ya Posta: S.L.P 97
Simu ya Mezani: +255-028-2810339
Simu: +255-028-2810339
Barua Pepe: ded@kasuludc.go.tz
Copyright ©2024 kasuludc . All rights reserved.